Wakutana mjini Iringa kuijadili SerikaliWANAFUNZI
waliofeli mtihani wa taifa wa kidato cha nne, wamekutana mjini Iringa.
Wanafunzi hao walikutana jana saa tano asubuhi, katika ukumbi wa
mikutano wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Mtakatifu Augustino cha Ruaha
(RUCO) kwa uratibu wa Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa
Iringa, Jesca Msambatavangu.
Katika mkutano huo, wanafunzi zaidi ya 400 kutoka maeneo
mbalimbali ya Mkoa wa Iringa, walijaa ukumbini na wengine walilazimika
kusimama nje ya ukumbi kwa kuwa ukumbini hakukuwa na nafasi.
Baada
ya mjadala kuanza, baadhi ya washiriki waliokuwa wakipewa nafasi ya
kuzungumza, walikuwa wakishindwa kujieleza, badala yake walikuwa wakilia
kuonyesha ni kwa jinsi gani wasivyoridhishwa na matokeo yao.
Wengine
badala ya kuonyesha masikitiko yao, walikuwa wakiishutumu Serikali wazi
wazi kwa kile walichokuwa wakisema kwamba wamefeli kutokana na uzembe
uliofanywa na waliosahihisha mitihani yao.
Hata hivyo,
wakizungumza katika kikao hicho, wanafunzi hao walisema licha ya Waziri
Mkuu, Mizengo Pinda, kuunda tume ya kuchunguza matokeo hayo, ikubali
kulegeza masharti ya kujiunga na vyuo vya ufundi na vyuo vinginevyo ili
waweze kupata elimu wanayoihitaji.
Mmoja wa wanafunzi hao, Gerald
Kiyeyeu, aliyehitimu kidato cha nne katika Shule ya Sekondari ya St.
Michael, alisema kwa kuwa baadhi yao wanaamini wamefelishwa, kuna haja
kwa Serikali kuruhusu mitihani hiyo isahihishwe upya ili ukweli halisi
upatikane.
Kwa mujibu wa Kiyeyeu, kama matokeo hayo yataachwa
kama yalivyo, wanafunzi wengi wataharibikiwa maisha, wakiwamo wanaotoka
katika familia masikini.
”Tunakuomba Mwenyekiti uzungumze na
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi (Dk. Shukuru Kawambwa) ili mitihani
yetu isahihishwe upya na wale wanaotaka kurudia mitihani yao
wagharamiwe na Serikali, kwa vile vituo vinavyotoa huduma hiyo vinatoza
gharama kubwa kuliko uwezo wetu,” alisema Upendo.
Naye Upendo
Vitus aliyehitimu katika Shule ya Sekondari Tagamenda, alimwambia
Mwenyekiti huyo wa CCM, kwamba wanachotaka wao Serikali iruhusu mitihani
isahihishwe upya ili ukweli ujulikane.
Alisema kwamba haoni umuhimu wa tume iliyoundwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kwa kuwa haitakuja na majibu yanayoaminika.
Kutokana
na hali hiyo, alisema kinachotakiwa ni Serikali kukubali mitihani hiyo
isahihishwe upya, ikiwa ni pamoja na kugharamia masomo kwa watakaotaka
kurudia kidato cha nne mwaka huu.
Naye Msambatavangu alipokuwa
akizungumza katika mkutano huo, aliwataka wanafunzi hao kutoyumbishwa na
kauli za wanasiasa, kwa kuwa wanasiasa wanaweza kuwatumia vibaya
kupitia matokeo mabaya ya kidato cha nne.
Pia, aliwataka baadhi
yao waliokuwa na mawazo ya kujiua, wasifanye hivyo japokuwa wazazi wao
wanawasema vibaya baada ya kufeli mtihani huo.
”Hakika hamtajuta
kwa uamuzi huu niliouchukua wa kukutana na nyie kwa sababu nimeumia sana
moyoni mwangu na nikalazimika kusema lazima kuna kitu kifanyike kwa
ajili yenu.
”Nimeshafanya mazungumzo na baadhi ya vyuo vikuu vya
hapa kama Tumaini na RUCO ili waangalie namna ya kuwasaidia kwa kuandaa
kozi za muda mfupi hadi mwezi Mei mwaka huu.
”Lengo la kuandaa kozi hizi ni kuwanoa ili baadaye tuone kama wapo wanaoweza kusaidiwa kwa kuendelea na elimu ya ngazi ya cheti.
”Najua
kuna wanasiasa pamoja na wanaharakati watajiingiza katika hili, lakini
tambueni kwamba, huu siyo wakati wa wanasiasa, wanaharakati na wadau wa
elimu nchini kupigana mawe kutokana na anguko hili.
”Ila
kinachotakiwa hapa ni Serikali ya CCM na watendaji wake, kujipanga upya
na kutazama ni kwa namna gani kundi la wanafunzi waliofanya vibaya
katika mitihani yao wanaweza kusaidiwa.
”Nayasema haya kwa sababu
inawezekana mliopata sifuri na kuonekana hamna maana, mkawa kioo katika
maisha na waliowacheka na kuwabeza, wakawaheshimu kutokana na mchango
wenu katika elimu hapo baadaye.
”Nawaomba sana msikate tamaa,
maisha ni safari ndefu kwa sababu kufeli mitihani si kufeli maisha,
unaweza ukafeli mtihani lakini kwa kuwa Mungu ana mipango yake kwa kila
mtu, unaweza kuwa mtu wa maana kuliko hata yule aliyefaulu,” alisema
Msambatavangu.
Naye Mkurugenzi wa Kozi Fupi na Masomo Endelevu
katika Chuo cha RUCO, Baby Chuma, aliwataka wanafunzi hao kutokata tamaa
kwa kuwa kufeli kidato cha nne siyo kufeli maisha.
Aliwataka pia
wajiendeleze kwa kujiunga na kozi mbalimbali za masomo ili baada ya
miaka miwili, wawe na sifa ya kujiunga na vyuo vikuu.
Katika
utekelezaji wa suala hilo, alisema menejimenti ya RUCO, imeshakubaliana
na kiongozi huyo wa CCM ili kozi fupi zitolewe kwa waliofeli mitihani
hadi Mei mwaka huu.
Kwa upande wake, Msajili wa Wanafunzi wa Chuo
Kikuu cha Tumaini (IUCo), Melckzedeck Nduye, aliwahakikishia wanafunzi
hao, kwamba chuo hicho kimeungana na wadau wengine kutoa huduma kwa
wanafunzi waliofeli kuanzia Machi, mwaka huu.
Wakati hao wakisema
hayo, Mratibu wa Uhamasishaji wa Baraza la Vijana wa Chama cha
Demokrasia na Maendeleo (BAVICHA), Wilaya ya Iringa, Aidan Salehe,
alipoulizwa kuhusu matokeo hayo ya kidato cha nne, alisema baraza hilo
limepanga kuwaunganisha wanafunzi hao kwa kuitisha maandamano ya kulaani
matokeo hayo.
”Maandamano yako pale pale, mazingira mabovu ya
elimu, mitaala mibovu na uongozi wa aina hii, ndio tunataka vijana
wausemee wenyewe.
”Katika hili alichokifanya Mwenyekiti wa CCM ni
kizuri kabisa na kinapaswa kupongezwa, lakini ukweli ni kwamba, ameamua
kuwakutanisha waliofeli kwa sababu anajua tukiandamana tunaweza kuchota
wanachama wengi zaidi wakiwamo wa CCM,” alisema Aidan.
Katika
matokeo hayo ya kidato cha nne yaliyotangazwa wiki iliyopita, Mikoa ya
Iringa na Njombe ilikuwa na wahitimu 15,428, lakini asilimia 89 walipata
alama sifuri.
Wakati akitangaza matokeo hayo, Dk. Kawambwa
alisema watahiniwa 480,036 walisajiliwa nchini kote kufanya mtihani
lakini waliofanya mtihani ni 397,136. Pia alisema jumla ya watahiniwa
126, 847 kati ya 397,136 waliofanya mtihani huo wamefaulu huku
watahiniwa 270,289 hawakufaulu.
Katika matokeo hayo, alisema
waliopata daraja la kwanza ni 1,641, daraja la pili ni 6,453, daraja la
tatu ni 15,426, na darala la nne ni 103,327.